Category Title

  • Government Budget Speeches
  • Ministry's Budget Speeches
  • Budget Books 2024/2025
  • Budget Books 2023/2024
  • Budget Books 2022/2023
  • Budget Books 2021/2022
  • Budget Books 2020
  • Budget Books 2018/2019
  • Budget Books 2015/2016
  • Budget Books 2014/2015
  • Content not found
  • Content not found
  • Content not found

MKAKATI WA MUDA WA KATI WA UKUSANYAJI MAPATO WAZINDULIWA

18 Sep, 2025
MKAKATI WA MUDA WA KATI WA UKUSANYAJI MAPATO WAZINDULIWA

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba (wa pili kulia), akiwa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango Zanzibar, Dkt. Juma Malik Akil (wa pili kushoto), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Christian Omolo (wa kwanza kulia) na Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Dkt. Fred Msemwa (wa kwanza kushoto), wakionesha Mkakati wa Muda wa Kati wa Ukusanyaji wa Mapato wa Miaka mitatu (Medium Term Revenue Strategy) baada ya hafla ya uzinduzi wa Mkakati huo uliopangwa kutekelezwa kuanzia mwaka 2025/2026 hadi 2027/2028, pamoja na Kamati za usimamizi na utekelezaji wa Mkakati huo, katika ukumbi wa Kambarage, Treasury Square, jijini Dodoma.

 

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, amezindua Mkakati wa Muda wa Kati wa Ukusanyaji wa Mapato wa Miaka Mitatu (Medium Term Revenue Strategy) uliopangwa kutekelezwa kuanzia mwaka 2025/2026 hadi 2027/2028 na Kamati za usimamizi na utekelezaji wa Mkakati huo.
 

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Mkakati huo, ukumbi wa Kambarage Wizara ya Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma, Dkt. Mwamba alisema kuwa Mkakati huo unalengo la kuweka msingi imara ya ukusanyaji wa mapato, kuweka utabirifu wa sera za mapato na kuongeza makusanyo ya mapato.
 
Alisema kuwa utekelezaji wa Mkakati huo utasaidia kuongeza uhiari wa ulipaji kodi, kutambua na kuziba mianya ya ukwepaji kodi, kupunguza nakisi ya bajeti na kuimarisha imani ya wananchi na uwekezaji katika mfumo wa mapato.
 
“Utekelezaji wa kazi hii utaboresha usimamizi wa mapato ya Serikali na kuhakikisha tunakuwa na bajeti endelevu itakayowezesha Serikali kuongeza kasi ya utoaji wa huduma muhimu kwa wananchi kwa kutumia mapato ya ndani”, alisema Dkt. Mwamba.
 
Dkt. Mwamba alisema kuwa Mkakati umeainisha maboresho ya mikakati na hatua mbalimbali ambazo zimekuwa zikiendelea kutekelezwa na Serikali katika kuhakikisha Serikali inakusanya  mapato  mengi  kutoka kwenye  vyanzo  vyake vya  ndani.  
 
Alisema kuwa hatua hizo zimegawanyika katika makundi matatu ambayo ni mapendekezo ya maboresho ya sera, maboresho ya usimamizi wa ukusanyaji wa mapato na maboresho ya Sheria.

Dkt. Mwamba alisema kuwa Mkakati huo ulioandaliwa na Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo washirika wa maendeleo na wadau wengine kutoka taasisi za Serikali na sekta binafsi, unapendekeza kuandaliwa kwa sera ya kodi kitaifa itakayotoa mwongozo wa kuandaa na kuboresha sera za kodi na  kuboresha mifumo ya kielektroniki inayotumika katika ukusanyaji wa mapato.

Alisema kuwa Mkakati huo utaongeza utii na uhiari wa ulipaji kodi, kuimarisha na kuboresha usajili wa walipakodi, kuboresha usimamizi wa misamaha ya kodi, kuboresha marejesho ya kodi, kuboresha viwango vya kodi, kuboresha na kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato yanayotokana na uchumi wa kidigitali na kuboresha usimamizi wa ukusanyaji wa mapato yanayotokana na forodha.

Kwa upande mwingine amewapongeza wajumbe wote walioteuliwa kwa kukubali uteuzi huo ili kushiriki katika kazi hiyo muhimu ambayo  imejumuisha wajumbe wenye ujuzi na uzoefu katika masuala ya uchumi, kodi na fedha kutoka Serikalini na sekta binafsi.
 
Kwa upande wake Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa  Sera, Wizara ya Fedha, Dkt. Jonson Nyella, alisema kuwa  uandaaji wa Mkakati ulianza na mashauriano yakiongozwa na wataalamu wa ndani na kisha Wataalamu kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF)  ambao walitoa msaada wa kiufundi.

Alisema kuwa Mkakati huo ni muhimu katika kupunguza nakisi ya bajeti na hivyo kuwezesha kugharamia miradi ya maendeleo kwa kupitia fedha za ndani, lengo ni kuisaidia nchi kujitegemea ikizingatiwa Nchi imetoka uchumi wa chini kwenda uchumi wa kati ambao unahitaji kujitegemea kwa kiasi kikubwa.

Mwenyekiti wa Kamati iliyozinduliwa ni  Katibu Mkuu Hazina  na Katibu ni   Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha anayesimamia Uchumi, Wajumbe wa Kamati ni pamoja na Katibu Mkuu Ofisi ya Mipango na Uwekezaji, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais  Fedha na Mipango Zanzibar, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI, Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Nyumba na Makazi, Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii na Katibu Mkuu Wizara ya  Mawasilino na Teknolojia ya Habari.

Wengine ni Gavana wa Benki Kuu, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Msajili wa Hazina, Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, rais wa Chemba ya Biashara,  Viwanda na Kilimo (TCCIA) na Mwenyekiti wa  Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF)

Utaratibu wa kuandaa na kutekeleza Mkakati huo umekuwa ukitumika katika nchi mbalimbali ikiwemo Kenya, Uganda, Malawi, Siera Leone, Ghana, Morocco na Rwanda.
 
Mwisho.