Category Title

  • Government Budget Speeches
  • Ministry's Budget Speeches
  • Budget Books 2024/2025
  • Budget Books 2023/2024
  • Budget Books 2022/2023
  • Budget Books 2021/2022
  • Budget Books 2020
  • Budget Books 2018/2019
  • Budget Books 2015/2016
  • Budget Books 2014/2015
  • Content not found
  • Content not found
  • Content not found

MHE. LUSWETULA AHIMIZA UADILIFU NA MATUMIZI YA TEKNOLOJIA KUIMARISHA UKAGUZI WA NDANI

13 Apr, 2026
MHE. LUSWETULA AHIMIZA UADILIFU NA MATUMIZI YA TEKNOLOJIA KUIMARISHA UKAGUZI WA NDANI

Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), akikabidhiwa tuzo na aliyekuwa rais wa Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani (IIA), Bi. Enna Victor, baada ya kufungua Mkutano wa Nne wa Wakaguzi wa Ndani, ulioandaliwa na Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani (IIA), katika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Cate, mkoani Morogoro.

 

Wakaguzi wa ndani nchini wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu, weledi na kwa kuzingatia maadili ya kazi ili kulinda maslahi ya Taifa na kuhakikisha fedha za Serikali zinatumika ipasavyo.

Maagizo hayo yalitolewa na Naibu Waziri wa Fedha Mhe. Laurent Deogratius Luswetula (Mb), kwa niaba ya Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), wakati akifungua Mkutano wa Nne wa Wakaguzi wa Ndani, ulioandaliwa na Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani Nchini (IIA), katika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Cate, mkoani Morogoro.

Alisema uadilifu ni nguzo kuu itakayowezesha taasisi za umma kutoa huduma bora na zenye tija kwa wananchi pamoja na kujenga mfumo imara wa udhibiti ambao utasaidia kuziba mianya ya upotevu wa fedha na kuongeza ufanisi katika matumizi ya mali za umma.

‘‘Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imechukua hatua madhubuti kuimarisha uwazi, kujenga imani ya umma, kuzuia rushwa, na kusisitiza uwajibikaji katika matumizi ya fedha hivyo wakaguzi wa ndani wana wajibu wa kusimamia matumizi sahihi ya rasilimali za umma’’, alisema Mhe. Luswetula.

Alisisitiza kuwa thamani ya umma inapatikana pale hatua za Serikali zinapopelekea uboreshaji wa huduma, matumizi bora ya rasilimali, kupungua kwa rushwa na ubadhirifu, na kuongezeka kwa imani ya wananchi.

‘‘Wakaguzi wa ndani wanachangia thamani hii kwa kuimarisha utawala, usimamizi wa vihatarishi, na mifumo ya udhibiti wa ndani kwa kutoa uhakiki huru na mapendekezo kwa ajili ya maboresho kuziwezesha taasisi za umma kufikia malengo yake kwa tija na kwa kufuata maadili’’, alifafanua Mhe. Luswetula.

Aidha, alisisitiza ushirikiano wa karibu na vitengo vya ukaguzi wa ndani katika kudhibiti rasilimali za umma, kulinda uhuru wa wakaguzi na kuhakikisha kuwa mapendekezo yanayotolewa baada ya ukaguzi yanafanyiwa kazi kikamilifu.  

Vilevile aliwaasa wakaguzi wa ndani kujiandaa na mabadiliko ya teknolojia kwa kujifunza matumizi ya takwimu, akili bandia, na mifumo ya ukaguzi wa kidijitali ili kusaidia kurahisisha kazi na kuleta matokeo ya haraka na sahihi.

Mhe. Luswetula alisema ana imani mkutano wa mwaka huu wenye kauli mbiu “Kuleta Matokeo kwa Pamoja: Ukaguzi wa Ndani kwa Ajili ya Thamani ya Umma” utaimarisha mchango wa ukaguzi wa ndani katika sekta ya umma, huku ukiwapa wajumbe wa Bodi na menejimenti mbinu za kivitendo za kutekeleza majukumu yao ya usimamizi.

‘‘Kaulimbiu hii inagusa kiini cha utumishi wa umma kutoa huduma bora kwa wananchi kupitia uwajibikaji, uwazi, na utawala bora. Inatazama mbele thamani ya ukaguzi wa ndani katika kuleta matokeo chanya pale unapofanya kazi kwa ushirikiano na wadau ili kubadilisha uhakiki, maarifa, na ushauri kuwa matokeo yanayoonekana’’, alisisitiza Mhe. Luswetula.

Awali akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi Kaimu Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Kenneth Nindie, alisema kuwa kujenga uwezo wakaguzi wa ndani ni muhimu katika kuboresha ukaguzi wa ndani nchini na kuwawezesha kuendana na mabadiliko ya teknolojia.

Alisema washiriki wa mkutano huo watapata mbinu za kiutendaji na ufahamu wa kina kuhusu namna ya kuboresha ufanisi kazini, huku wakipata nafasi ya kubadilishana uzoefu na kujifunza kutoka kwa wataalamu wengine wa sekta hiyo.

Naye Rais na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani Nchini (IIA), Jonathan Ngoma, amesema mkutano huo umelenga kuwaleta pamoja wadau mbalimbali kujadili masuala ya uongozi bora na namna ya kuimarisha mifumo ya ukaguzi wa ndani nchini.

Mkutano huo uliwakutanisha viongozi wa Serikali, wajumbe wa menejimenti, wakaguzi wa ndani, wahasibu, wataalamu wa fedha, na wadau muhimu ili kutafakari, kujifunza, na kushauriana jinsi tunavyoweza kuendelea kuimarisha utawala bora, uwajibikaji, na uwazi katika sekta ya umma.

MWISHO.