TANZANIA KUONGEZA UWEKEZAJI KATIKA SEKTA ZA KIPAUMBELE
Serikali ya Tanzania inalenga kuongeza uwekezaji katika sekta za kipaumbele ikiwemo sekta ya Elimu, Afya, na Kilimo cha kisasa kinachozingatia mabadiliko ya Tabia nchi ili kuchochea ukuaji wa Uchumi Endelevu na Kupunguza Umaskini.
Hayo yamesemwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa niaba ya Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati akifungua Mkutano wa Kimataifa wa Tathmini ya Muda wa Kati wa Mzunguko wa 20 wa Benki ya Dunia (IDA20 Mid-Term Review) unaohusisha wakopaji, nchi Wahisani na Menejimenti ya Benki ya Dunia, unaofanyika kwa siku tatu, Zanzibar, ambapo pamoja na mambo mengine utajikita kufanya tathmini ya miradi inayotekelezwa katika nchi zenye kipato cha chini kupitia fedha za mkopo na msaada zinazotolewa na Mfuko huo uliopo chini ya Benki ya Dunia.