Category Title

  • Government Budget Speeches
  • Ministry's Budget Speeches
  • Budget Books 2024/2025
  • Budget Books 2023/2024
  • Budget Books 2022/2023
  • Budget Books 2021/2022
  • Budget Books 2020
  • Budget Books 2018/2019
  • Budget Books 2015/2016
  • Budget Books 2014/2015
  • Content not found
  • Content not found
  • Content not found

TANZANIA NA CITIBANK KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI

27 Jul, 2026
TANZANIA NA CITIBANK KUIMARISHA USHIRIKIANO WA KIMKAKATI

Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (MB) (kushoto), akisalimiana na Afisa Mkuu Mtendaji wa CitiBank, anayesimamia eneo la Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Bw. Akin Dawodu, katika ziara yake rasmi ya kiserikali kuimarisha ushirikiano na taasisi za kifedha za kimataifa na wawekezaji, jijini London nchini Uingereza.

Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Balozi Khamis Mussa Omar (MB), amefanya mkutano wa kimkakati jijini London nchini Uingereza na maafisa wakuu wa Citibank chini ya uongozi wa Bwana Akin Dawodu, Afisa Mkuu Mtendaji anayesimamia eneo la Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, katika ziara yake rasmi ya kuimarisha ushirikiano na taasisi za kifedha za kimataifa na wawekezaji.

Viongozi hao walipitia ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Citibank tangu ianze shughuli zake  nchini Tanzania mwaka 1995, na kujadili sifa za uwezo wa nchi kukopesheka katika soko la fedha la kimataifa, Eurobond ya kwanza inayokusudiwa kufunguliwa na Serikali siku za usoni, ufadhili wa mabenki ya mikopo ya usafirishaji (ECA), miradi ya miundombinu, marekebisho ya soko la mtaji pamoja na kuhamasisha uwekezaji wa sekta binafsi.

Citibank ilithibitisha tena nia yake ya kuendelea kushirikiana na Tanzania kuyafikia  masoko ya kimataifa ya mtaji, ukuaji wa masoko ya mtaji ya ndani, ushirikiano na wawekezaji barani Ulaya, Marekani, Mashariki ya Kati na Asia, na ufadhili wa miradi ya kimkakati ya miundombinu.

Katika mkutano huo uliowashirikisha pia Balozi wa Tanzania nchini Uingereza Mhe. Balozi Mbelwa Kairuki na Kamishna anayesimamia Idara ya Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justne, Mhe. Balozi Omar alieleza  kuhusu maendeleo ya hivi karibuni ya kiuchumi, ikiwa ni pamoja na ongezeko kubwa la uwezo wa uzalishaji wa umeme, ukarabati wa Bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, na upanuzi wa miundombinu ya usafiri wa anga.

Alieleza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo (Dira 2050) imeanza kutekelezwa rasmi kuanzia Julai mos mwaka 2026, ikilenga uchumi wa wa Tanzania kufikia dola za Marekani trilioni 1 katika miaka ishirini na tano ijayo, ambapo takriban asilimia 70 ya uwekezaji unahitajika kutoka sekta binafsi.

Alieleza pia kwamba mazungumzo kuhusu mradi wa kuchakata gesi asilia LNG, wenye thamani ya takriban dola bilioni 42 za Marekani, na wawekezaji yamekamilika kwa kiasi kikubwa, na kwamba Serikali na wawekezaji wamefikia makubaliano juu ya mfumo mkuu wa uendeshaji, na mradi unatarajiwa kuanza mara baada ya masuala yanayosalia ndani ya washirika yatakapokamilika.

Kuhusu marekebisho ya kodi na mazingira ya biashara, Mhe. Balozi Omar alisema kwamba Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliunda Tume, moja kiangazia  mazingira ya biashara na nyingine ya mfumo wa kodi, ambayo imewasilisha mapendekezo 284 ya namna ya kuboresha mifumo ya kodi ambayo Srikali inayafanyiakazi.

Alisisitiza kwamba marekebisho yajayo yatazingatia upanuzi wa wigo wa kodi, uboreshaji wa utawala na kuweka jitihada kubwa ya kukusanya rasilimali za ndani  badala ya kuongeza mizigo ya kodi.

Mhe. Balozi Omar alipendekeza kuanzishwa kwa mfumo rasmi wa ushirikiano wa kimkakati na Citibank, ukihusisha masoko ya mtaji ya umma, ufadhili wa miundombinu, ufadhili wa mabenki ya mikopo ya usafirishaji, mahusiano na wawekezaji, ukuaji wa soko la mtaji la ndani, kuhamasisha uwekezaji wa sekta binafsi na marekebisho ya utawala wa kodi.

Mwisho