Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), pamoja na viongozi mbalimbali wa Mamlaka ya Mapato Tanzania wakiongozwa na Kamishna Mkuu wa TRA, Bw. Yusuph Juma Mwenda pamoja na wananchi wakimshuhudia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, akizindua rasmi mbio na matembezi ya shukrani kwa walipakodi kuelekea Tuzo ya Rais kwa Mlipakodi Bora pamoja na maadhimisho ya miaka 30 ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) yatakayofanyika tarehe 1 Julai 2026, hafla inayolenga kutambua mchango wa walipakodi katika maendeleo ya taifa na kuhamasisha.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, akiongoza kikao kati ya Serikali ya Tanzania na Ujumbe wa Benkiy a Dunia uliyoongozwa na Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia, Bw. Firas Raad, ambapo walijadili kuhusu miradi ya kipaumbele ya Serikali itakayofadhiliwa na Benki ya Dunia kupitia Mzunguko wa 21 (IDA-21), kwa lengo la kuharakisha utekelezaji wa agenda ya maendeleo ya Taifa, kilichofanyika ofisi za wizara jijini Dodoma.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo, wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi waandamizi wa Wizara ya Fedha na Wizara ya Mipango na Uwekezaji, baada ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitisha kwa kishindo Bajeti Kuu ya Serikali ya Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa asilimia 97.66 baada ya wabunge 385 kupiga kura ya ndio kuunga mkono Bajeti hiyo.
Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB) zimekubaliana kuharakisha hatua za kukamilisha mikataba ya ufadhili wa Mradi wa Maji Safi na Usafi wa Mazingira wa Jiji la Mwanza Awamu ya Pili (LV WATSAN II), unaolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za maji safi na usafi wa mazingira kwa wananchi wa Mkoa wa Mwanza na maeneo jirani.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Balozi wa Uturuki nchini, Mhe. Balozi Dkt. Bekir Gezer, wakibadilishana Mikataba ya Kuondoa Utozaji wa Kodi Mara Mbili na Kuzuia Ukwepaji wa Kodi katika Mapato (DTA), baada ya kusaini mikataba hiyo katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Hyatt Regency, jijini Dar es Salaam, ambapo hatua hiyo inatarajiwa kuchochea uwekezaji na biashara kati ya mataifa hayo mawili.
Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mlipaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Natu El-maamry Mwamba na Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Standard Chartered, Bw. Herman Kasekende, wakisaini Mkataba wa kugharamia ukamilishaji wa Reli ya Kisasa (Standard Gauge -SGR), kipande cha tatu (loti 3) na cha nne (loti 4) kutoka Makutupora ya mkoani Singida hadi Isaka, yenye thamani ya takriban dola za Marekani bilioni 1.277, katika hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kambarage, Treasury Square, jijini Dodoma.
Tanzania imejipanga kikamilifu kuwa kitovu cha uwekezaji barani Afrika na inawakaribisha wawekezaji wa Marekani kuchangamkia fursa lukuki zilizopo katika sekta mbalimbali za uchumi.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) wakati alipoongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa Uwekezaji ulioandaliwa na Baraza la Biashara la Kimataifa- Business Council for International Understanding (BCIU), uliofanyika katika Ofisi za BCIU, jijini Washington D.C nchini Marekani, pembezoni mwa Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, ameshiriki katika hafla ya kifungua kinywa iliyowakutanisha wanawake viongozi kutoka sekta mbalimbali, iliyoandaliwa na Benki ya Dunia kupitia Wakurugenzi Watendaji wake, Bi. Anna Bjerde na Bi. Anshula Kant, katika Ofisi za Benki hiyo jijini Washington D.C nchini Marekani, kando ya Mikutano ya Majira ya Kipupwe ya Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa-IMF inayoendelea jijini humo.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar, ameishauri Benki ya Dunia kuangalia namna ya kuiwezesha sekta binafsi katika nchi za Afrika ili iweze kuwa imara na kuchangia kukuza uchumi wa nchi hizo.
Mhe. Balozi Omar, ametoa wito huo wakati akichangia mada katika mkutano wa Kundi la Kwanza la nchi za Kanda ya Afrika, wanachama wa Benki ya Dunia (Africa Group 1 Constituency), uliofanyika Makao Makuu ya Benki hiyo, Jijini Washington D.C, nchini Marekani.
Tanzania imeendelea kuimarisha ushirikiano wake na Benki ya Uwekezaji wa Miundombinu ya Asia (AIIB), hatua inayotarajiwa kufungua fursa mpya za ufadhili kwa miradi ya kimkakati ya maendeleo, ikiwemo maji, nishati, usafiri, teknolojia ya habari na Mawasiliano pamoja na miundombinu ya kijani.